Friday, November 27, 2015

Tafakari: Marko 11:25 "Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu".

Kama kuna dhambi itakayowapeleka wengi motoni, ni hii ya kutosamehe. Ingelikuwa mtu anapewa kuona yaliyo ndani ya mioyo ya watu; tungeshuhudia majeraha makubwa yasiyopona, yaliyotokana na kuumizwa na ndugu au jamaa na wakati mwingine wapenzi wao. Japokuwa hatuwezi kuona, maneno ya manung'uniko na malalamiko yanafunua mizigo ilioko ndani japo kwa sehemu ndogo.

Wengi utasikia wanasema "nimemsamehe ila sitasahau" huyo bado anamaumivu hajasamehe. Wengi wanaenda majumba ya Ibada, wanaimba, wanahubiri, wanatoa zaka na sadaka, huku wakiwa bado wana mafukuto ya chuki kwa waliowakosea. Utakuta mtu anajisifia akisema "mimi hata simsalimii" au "nikimuona nakereka", ndivyo wengi walivyo hata kama hawasemi. Jiulize ukimuona yule mbaya wako unajisikiaje? Kila mmoja analo jibu.

Haijalishi umeumizwa kiasi gani; iwe ni kazini, iwe kwenye ndoa au mahusiano, au katika mazingira yoyote; unapaswa kusamehe kabisa, na kuachilia roho za kulipa kisasi, manung'uniko, malalamiko, chuki, hasira na harara. Hayo yote yakidumu moyoni yanafunga kabisa milango ya mbinguni.

Yesu alirudia kufundisha jambo hili akiwa anawafundisha wanafunzi wake kuomba akisema - Mathayo 6:12 "utusamehe deni (makosa) yetu, kama sisi nasi tuwasemehevyo wadeni (waliotukosea) wetu". Kwa maneno hayo, tunajifunga kitanzi au kuwa huru, kwa kusamehe au kutosamehe.

Wapendwa katika hali ya ubinadamu jambo hili la msamaha ni gumu, hivyo linahitaji kutoa maisha yetu kwa Yesu Kristo ili atupatie uwezo wa kutenda yale tusiyoweza, atupatie tabia ya Upendo wa kuwapenda wabaya na kuwaombea. Msamaha ni mojawapo ya vipimo kama kweli tunaongozwa na Roho mtakatifu au bado tuko chini ya kongwa la utumwa.

NAWATAKIA WOTE SIKU NJEMA YENYE NURU YA MAFANIKIO NA BARAKA TELE.

By: Ev. Eliezer Mwangosi - 0767 210 299.
****TUMA PICHA NA VIDEO WhatsApp 0713 059 073 NA 0717 367 693***
Categories:

0 comments:

Post a Comment

SIKILIZA NA DOWNLOAD WIMBO "KIFO" TOKA KWA PADACK

MAHUBIRI YA USHINDI HATIMAYE 2017 HAYA HAPA