Dhambi
ilikata mawasiliano kati ya Mungu na mwanadamu, lakini kwa upendo
wake Mungu alitafuta njia nyingine ya mawasiliano. “Kisha
akawaambia, Sikilizeni basi maneno yangu; akiwapo nabii kati yenu,
Mimi, BWANA, nitajifunua kwake katika maono, nitasema naye katika ndoto”
(Hes.12:6). Nabii akiwa katika maono macho yake yanatazama na kuona
mambo ambayo Mungu anamwonesha; watu wengine walio karibu naye hawawezi
kuona mambo hayo; waweza kusikia sauti au tetemeko (Dan.10:7;
Mdo.9:3-7). Ndoto huja usiku anapolala; anaoneshwa mambo fulani muhimu
anayopaswa kuwaambia watu wa Mungu au kuwaonya mataifa. Wakati mwingine
Mungu anamtuma malaika wake na ujumbe maalumu kwa nabii (Dan.9:20-23;
Ufu.19:9,10)
Mungu
hawezi kuliangamiza taifa lo lote bila kuwasiliana na manabii wake ile
watoe onyo mapema kusudi watu wale wajirekebishe nyendo zao.
“Hakika Bwana Mungu hatafanya neon lo lote bilz kuwafunulia watumishi
wake manabii siri yake” (Amosi 3:7). Nuhu, Ibrahimu na Yona
walipewa ujumbe maalumu wa maangamizi ya wanadamu na walitoa
onyo. Waliojirekebisha hawakuangamizwa; wale waliokataa kujirekebisha
waliangamizwa (Yer.18:7-10; Mwanzo Sura ya 18 na 19; Yuda 7; 2
Pet.2:6; Yona 3 hadi 4:1). Dunia hii ya sasa inafanana na Sodoma na
Gomora na manabii wanatupasha habari kuwa itateketezwa kwa moto kama
Sodoma na Gomora (2 Pet.3:1-7,10).
Kwa kuwa sisi ni watu wa kawaida, hatujui Mungu anakusudia
kufanya
nini hapa duniani, ni jambo la muhimu mno kuwasikiliza manabii
wake. “Angalieni msimkatae yeye anenaye. Maana ikiwa hawakuokoka wale
waliomkataa yeye aliyewaonya juu ya nchi, zaidi sana
hatutaokoka sisi tukijiepusha na yeye atuonyaye kutoka mbinguni”
(Ebr.12:25,26). Mungu ndiye anayewapasha habari za matukio duniani
manabii wake. Hivyo tutapata hasara sisi wenyewe tukiwapuuzia, wala
hatutafanikiwa katika safari yetu ya mbinguni. “…mwaminini BWANA,
Mungu wenu, ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo
mtakavyofanikiwa” (2 Nya.20:20).
Haitoshi kujihami na kusema kila nabii anayekuja ni nabii wa uongo maana
manabii
wa kweli wapo pia hadi mwisho wa dunia (1 Kor.12:28; Efe.4:8,11-14).
Je, kanisa limefikia umoja wa imani sasa? Hapana. Je, kanisa
limefikia cheo cha kuwa na tabia kama ile ya Yesu? Hapana. Je,
waumini wanamfahamu sana Yesu? Hapana. Kwa ajili hiyo tunawahitaji
manabii na wahudumu wengine kutoa huduma yao ndani ya kanisa la Mungu.
Unabii wa Yoeli 2:28-32 ulitimia kwa sehemu tu siku ile ya Pentekoste
(Mdo.2:17-21). Kumwagwa kwa Roho Mtakatifu siku ya Pentekoste ni “mvua
ya vuli.” Tunangojea “mvua ya masika” Roho Mtakatifu
atakapomwagwa tena itakapotangazwa Amri ya Jumapili kwa ulimwengu mzima
na kulazimishwa (Ufu.13:16,17; 18:1-4). Uwezo wa Roho Mtakatifu utakuwa
mara kumi kuliko ule wa Pentekoste na watu wa Mungu waliodanganywa
watarudi katika zizi la Kristo (Ufu.18:4; Yn.10:16).
Ni kweli Yesu alionya, akisema, “Jihadharini na manabii wa uongo, watu
wanaowajia
wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali.
Mtawatambua kwa matunda yao” (Mt.7:15,16). Wamo ndani ya makanisa,
wanatumia jina la Yesu, lakini wametumwa na Shetani kuwadanganya
wateule ili wapotee na kujitenga mbali na Mungu (1 Kor.11:13-15;
Yer.14:14:16; Mt.24:11,24; 7:15-23). Habari njema ni kwamba
tutawatambua. Viko vipimo vikuu vinne vya kuwapima manabii kama
wametumwa na Mungu au na Shetani. Lazima nabii atimize vyote vinne,
akishindwa kimoja hafai.
🔷Kipimo Cha Kwanza:
Sheria
na Ushuhuda (Isa.8:20). Wapimwe kwa Amri Kumi za Mungu, pia
mafundisho yao yapimwe kwa Biblia. “Na waende kwa Sheria na
Ushuhuda; ; ikiwa hawasemi sawasawa na neon hili, bila shaka kwa hao
hapana asubuhi” (Isa.8:20). Wakivunja moja tu wamevunja zote
(Yak.2:10-12). Karibu zaidi ya asilimia tisini na tano ya manabii
watatupwa mbali kwa kipimo hiki peke yake; hata mtu asiyeijua Biblia
anaweza kuwapima bila shida. Kwa vile Amri za Mungu zimebadilishwa, hapa
nanukuu kama zilivyotangazwa mlimani Sinai:
1⃣ Usiwe na miungu mingine ila Mimi.
2⃣
Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho
juu mbinguni, wala kilicho chini duniani; kwa kuwa mimi, BWANA, Mungu
wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata
kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao, nami nawarehemu maelfu
elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu.
3⃣ Usilitaje bure jina la BWANA, Mungu wako, maana BWANA hatamhesabia kuwa hana hatia mtu alitajaye jina lake bure.
4⃣
Ikumbuke siku ya sabato uitakase. Siku sita fanya kazi, utende
mambo yako yote; lakini siku ya saba ni sabato ya BWANA, Mungu wako,
siku hiyo usifanye kazi yo yote, wewe, wala mwana wako, wala
binti yako, wala mtumwa wako, wala mjakazi wako, wala mnyama wako wa
kufuga, wala mgeni aliye ndani ya malango yako. Maana, kwa siku sita
BWANA alifanya mbingu, na nchi, na bahari, na vyote vilivyomo,
akastarehe siku ya saba; kwa hiyo BWANA akaibarikia siku ya sabato
akaitakasa.
5⃣ Waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na BWANA, Mungu wako.
6⃣ Usiue.
7⃣ Usizini.
8⃣ Usiibe.
9⃣ Usimshuhudie jirani yako uongo.
Usiitamani nyumba ya jirani yako, usimtamani mke wa jirani yako; wala
mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng’ombe wake, wala punda wake, wala
cho chote alicho nacho jirani yako.
Manabii wengi wanaojitapa Kipimo hiki tu kinawatupa nje
🔷Kipimo cha Pili:
Matunda
au Maisha yao (Mt.7:20). “Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua”
(Mt.7:20). Hiki si rahisi mpaka uwe umekaa na nabii huyo kwa
kipindi fulani na kujua tabia yake. Lakini yaliyo moyoni mwa mtu
mara nyingi yanatoka kinywani mwake na kudokeza tabia yake. Pia
mafundisho yake yapimwe kama yanawafanya watu wamjue Yesu zaidi au
yanawapeleka mbali naye. Maisha ya anasa ulevi na mambo ya ajabu
hutayasikia katika maisha yake daima hutafuta utukufu wa Mungu sio wa
kwake.
♦Kipimo cha Tatu:
Kukubali kuwa Yesu alikuwa na mwili kama wetu (1 Yoh.4:1-3).
“Wapenzi,
msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na
Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani. Katika
hili mwamjua Roho wa Mungu; kila roho ikiriyo kwamba Yesu
Kristo amekuja
katika mwili yatokana na Mungu. Na kila roho isiyomkiri Yesu haitokani na Mungu.
Na hii ndiyo roho ya Mpinga Kisto ambayo mmesikia kwamba yaja...” (1
Yoh.4:1-3).
Yesu asingetusaidia kitu kama angekuwa na mwili tofauti na wetu, maana
angetumia nguvu za Mungu kushinda majaribu. Habari njema ni
kwamba alikuwa na mwili kama wetu, hivyo anaweza kutusaidia
(Ebr.2:14-18; 4:14-16; Yn.1:1-3,10,14).
🔷Kipimo cha Nne:
Unabii
Uliotimia (Yer.28:9). “Nabii atabiriye habari za amani, neno la
nabii yule litakapotokea, ndipo nabii yule atakapojulikana, kuwa BWANA
amemtuma kweli kweli” (Yer.28:9). Lakini tahadhari kubwa! “Kukizuka
katikati yako nabii, au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu,
ikatukia hiyo ishara au hiyo ajabu aliyokuambia, akisema, Na tuifuate
miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo; wewe usiyasikize maneno ya
nabii yule, au yule mwotaji wa ndoto; kwa kuwa BWANA, Mungu wenu,
yuawajaribu, apate kujua kwamba mwampenda BWANA, Mungu wenu, kwa
mioyo yenu yote na roho zenu zote…” (Kum.13:1-11).
Tumeona
manabii wengi wakiwatabiria maraisi mbalimbali na unabii wao
haukutimia, wengine wanatabiria vifo wengine, na mambo mengi ya ajabu
tunayoendelelea kuyaona sasa
🏾ZINGATIA:
Kufanya miujiza kwa jina la Yesu sio kithibitisho cha unabii maana hata manabii wa uongo hufanya miujiza
🔷Mathayo
7:21-23 Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika
ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye
mbinguni. Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii
kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya
miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe;
ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.
🔷Ufunuo 13:13 Naye afanya ishara kubwa, hata kufanya moto kushuka kutoka mbinguni uje juu ya nchi mbele ya wanadamu.
♦Usiwaogope manabii au mitume, wapime kwa vipimo hivyo vinne, utawatambua walio wa kweli na wa uongo♦
****TUMA PICHA NA VIDEO WhatsApp 0713 059 073 NA 0717 367 693***
0 comments:
Post a Comment